Jeshi la Polisi nchini Sudan limetangaza kuwa, askari polisi wapatao
elfu sabini wameanza kupewa mafunzo maalumu kwa minajili ya kulinda
usalama katika majimbo yote, wakati wa kufanyika uchaguzi mkuu nchini
humo. Brigedia Siddiq Abdullah Abdulqadir, afisa mwandamizi wa jeshi la
polisi la Sudan amesema kuwa, licha ya askari polisi, wanajeshi, vyombo
vya usalama na taasisi za kiraia nazo zitashirikishwa katika kusimamia
mwenendo mzima wa uchaguzi wa rais na bunge nchini humo. Brigedia
Abdulqadir ameongeza kuwa, askari polisi hao watakuwa na jukumu la
kulinda usalama wa majimbo, usalama wa wagombea wa nafasi za urais na
ubunge pamoja na vituo vya kupigia kura. Wakati huohuo, Hussein Yassin
Hamad, Gavana wa Jimbo la Blue Nile amesisitiza kuwa, uchaguzi mkuu
utafanyika katika tarehe iliyopangwa. Gavana wa Blue Nile amevitaka
vyama vyote vya siasa na wananchi wa Sudan kutekeleza majukumu yao kwa
mujibu wa katiba ya nchi. Uchaguzi wa rais na bunge nchini Sudan
umepangwa kufanyika tarehe 13 ya mwezi ujao wa Aprili.
0 comments:
Post a Comment