
Waziri wa Ulinzi wa Uganda amesema kuwa, wanajeshi wa Marekani walioko
Jamhuri ya Afrika ya Kati wamemkabidhi kwa vikosi vya serikali ya
Uganda vilivyoko nchini humo Meja Jenerali Dominic Ongwen mmoja kati ya
makamanda wa ngazi za juu wa kundi la waasi wa Lord's Resistance Army
LRA wa nchini Uganda. Dakta Chrispus Walter Kiyonga amesema kuwa,
Kamanda Ongwen anayetafutwa kwa udi na uvumba na Mahakama ya Kimataifa
ya Jinai ICC, anakabiliwa na tuhuma za kutenda jinai za kivita. Hata
hivyo, Waziri wa Ulinzi wa Uganda hakubainisha wazi iwapo Meja Jenerali
Dominic Ongwen atafunguliwa mashtaka nchini Uganda au atapelekwa Hague,
nchini Uholanzi makao makuu ya ICC. Kundi la waasi wa LRA linaloongozwa
na Joseph Kony kwa zaidi ya muongo mmoja sasa limekuwa likitenda jinai
za kivita na zilizo dhidi ya binadamu nchini Uganda na hata nje ya
mipaka ya nchi hiyo, na kuleta hali ya hofu na wasiwasi katika mipaka ya
nchi za Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Jamhuri ya
Afrika ya Kati. Wakati hayo yakijiri, Shirika la Kutetea Haki za
Binadamu la Human Rights Watch limeeleza kuwa, kutiwa mbaroni Kamanda
Ongwen ni fursa nzuri ya kutekelezwa misingi ya haki za binadamu dhidi
ya jinai zinazofanywa na waasi wa LRA. Shirika hilo limetaka kamanda
huyo afunguliwe mashtaka haraka iwezekanavyo.
0 comments:
Post a Comment