Wednesday, 24 September 2014

Jumatatu ya tarehe 22 Septemba wawakilishi wa serikali na wapinzani wa Sudan Kusini walianza duru mpya ya mazungumzo ya amani katika viunga vya mji mkuu wa Ethiopia Addis Abab. Hii ni mara ya kwanza kwa pande mbili hizo hasimu za Sudan Kusini kukutana tangu yalipotiwa saini makubaliano ya nne ya usitishaji vita mwishoni mwa mwezi uliopita. Jumuiya ya Ustawi ya nchi za mashariki mwa Afrika IGAD ndiyo msimamizi wa mazungumzo ya amani ya Sudan Kusini ambayo tangu yalipoanza yamekuwa na mwendo wa kinyonga. Mada kuu katika duru hii mpya ya mazungumzo ni kuundwa serikali ya mpito na ya umoja wa kitaifa. Suala la kuchaguliwa Rais na Waziri Mkuu ni ajenda nyingine muhimu katika duru hii ya mazungumzo ya amani ya Sudan Kusini huko Ethiopia.
Wachambuzi wa mambo wanaamini kuwa, kuchaguliwa Rais na kuainishwa nguvu na mamlaka ya Waziri Mkuu kitakuwa kibarua kigumu mno hasa kwa kutilia maanani historia ya vita vya kuwania madaraka kati ya Rais wa sasa Salva Kiir na Riek Machar aliyekuwa Makamu wa Rais na ambaye kwa sasa ndiye kiongozi mkuu wa upinzani. Taban Deng Gai, mkuu wa timu ya wapinzani katika mazungumzo na serikali ya Juba ameituhumu serikali kwamba, imekiuka makubaliano ya usitishaji vita. Kwa upande wake serikali ya Sudan Kusini nayo inamtuhumu kiongozi wa upinzani Riek Machar kwamba,  amekiuka vipengee vya hati ya makubaliano. Nchi changa zaidi barani Afrika ya Sudan Kusini ilitumbukia katika dimbwi la machafuko kuanzia Desemba mwaka jana baada ya kuzuka mapigano kati ya wanajeshi wa serikali na wale watiifu kwa aliyekuwa Makamu wa Rais Riek Machar. Mapigano hayo yalienea kwa kasi kubwa na kugubika nchi yote. Hata kutiwa saini makubaliano ya usitishaji vita hakujawa dawa mujarabu, kwani mara kadhaa hati ya makubaliano hayo imekiukwa; na hivyo kushuhudiwa mapigano yakiendelea. Ni kwa kuzingatia kuweko kizungumkuti hicho, ndiyo maana hata suala la uundwaji wa serikali ya umoja wa kitaifa nalo limeakhirishwa. Wapembuzi wa masuala ya kisiasa wanaamini kuwa, vita vya madaraka kati ya Salva Kiir na Riek Machar ndicho chanzo cha kuibuka machafuko katika nchi hiyo changa ambayo ilitangaza rasmi kujitenda na Sudan Kuu Julai 2011. Mbali na machafuko, kwa sasa Sudan Kusini kama wanavyosema wataalamu wa Umoja wa Mataifa inakabiliwa pia na upungufu mkubwa wa chakula. Wataalamu wa Umoja wa Mataifa wanasema kuwa, hali ya upungufu wa chakula inayokabiliwa nayo Sudan Kusini ni mbaya mno ikilinganishwa na maeneo mengine duniani yanayotaabika na hali hiyo. Fauka ya hayo, mashirika ya utoaji misaada yametoa indhari kuhusiana na nchi hiyo kukumbwa na ukame. Ni kwa kuzingatia matatizo mbalimbali yanayoikabili Sudan Kusini ndio maana wachambuzi wa mambo wanasema kuwa, kuna haja kwa mgogoro wa kisiasa wa nchi hiyo kupatiwa ufumbuzi haraka iwezekano, ili kwa njia hiyo kuandaliwe uwanja wa kuyashughulia matatizo mengine yanayoikabili nchi hiyo.

Related Posts:


0 comments:

Post a Comment

Translate

facebook

TANGAZA HAPA

KWA HABARI MAKINI

Napokea maoni muhimu kwa pale unapoona apakustahili kuwepo kwenye blogg yetu makini yenye lengo la kukuunganisha pamoja na kuelimishana kwa yale mazuri yote piga simu kwa chochote muhimu namba zipo apo juu